Marehemu Samweli Sitta |
Lakini, kama hiyo ni kweli na kama ni kweli kwamba sisi sote binadamu, tupende tusipende, tumetekwa na ulazima wa kushiriki au kushirikishwa katika siasa kwa namna moja au nyingine, wapo baadhi yetu ambao wao ni wanyama wa kisiasa kuliko walivyo wanyama wa kisiasa wengine. Katika kundi hili, yumo Samuel John Sitta, spika wa zamani wa Bunge la Tanzania, mbunge wa Urambo na waziri katika wizara kadhaa za awamu nne za kwanza za serikali ya Jamuhuri ya Muungano ya Tanzania.
Nilikutana na Sitta kwa mara ya kwanza Agosti mwaka 1966. Wakati huo nilikuwa nasoma kidato cha nne katika shule ya serikali Nyakato, Bukoba, na nikiwa ni mwakilishi wa shule yangu katika mkutano mkuu wa National Union of Tanzanian Students (NAUTS), umoja wa wanafunzi wa Tanzania. Pamoja nami kutoka shuleni Nyakato alikuwa ni Ahmed Kiwanuka, hivi sasa mwanazuoni maarufu.
Sitta alikuwa ndiye kiongozi mkuu wa NAUTS, mwenyekiti, na alikuwa pia ni rais wa serikali ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (USUD). Wkati huo alikuwa anajiandaa kuachia ofisi zote mbili kwa kuwa alikuwa anakaribia kumaliza masomo yake. Mwishoni mwa mkutano huo wa 1966, katika nafasi ya mwenyekiti wa NAUTS, Sitta alirithiwa na Onesfore Chawe kutoka Chuo cha Ualimu Chang’ombe.
Mkutano mkuu wa 1966 uligubikwa na malumbano makali kati ya serikali ya Tanzania na umoja huo wa wanafunzi, ubishi mkuu ukiwa ni kuhusu mpango uliokuwa unaandaliwa wakati huo wa kuasisi programu ya lazima kwa wahitimu wa vyuo vikuu kutumika ndani ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Umoja wa wanafunzi ulilalamikia masharti ya maisha yaliyokuwa yakipendekezwa kwa wahitimu hao, ikiwa ni pamoja na kukatwa mishahara yao, kuishi kambini kwa kipindi cha miaka miwili na kuishi maisha ya kijeshi kwa kipindi hicho. Viongozi wa wanafunzi waliona kama vile walikuwa wanaonewa kuingizwa katika maisha magumu na kunyimwa sehemu ya mshahara wao.
Rais wa Jamuhuri, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alikuja kufunga mkutano huo na akajibu maswali ya washiriki; mojawapo lilihusu JKT. Miongoni mwa mambo aliyoyagusia muulizaji swali alitaja matatizo ya vijana wadogo wanaomaliza vyuo, hawana fedha na pengine wana majukumu ya kifamilia, halafu wanakatwa asilimia 60 ya mishahara yao.
Nyerere alilipuka na kufoka kwa mshangao, akisema ni kwa nini vijana wanaona ugumu wa kwenda kufanya kazi vijijini kuinua hali za maisha ya ndugu zao… badala yake wanadai “60 per cent! Sixty percent of what nonsense? You haven’t even received your first salary and already you are counting 60%? I think we made a mistake… at graduation you have no salary…..”
Miezi miwili baadaye, mwezi Oktoba, wanafunzi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam waliandamana kupinga JKT, wakaenda Ikulu, wakakusanywa, wakahutubiwa na Mwalimu katika hotuba iliyolenga kuwashitaki kwa wananchi, kisha wakafukuzwa chuo na kusombwa kurejeshwa majumbani kwao katika mikoa mbalimbali. Wengi wao hawakurudi kumaliza masomo yao hadi miaka mitatu baadaye, ikiwa ni pamoja na Sitta.
Ni muhimu kusema kwamba wakati wanafunzi wanaandamana, Sitta alikuwa amestaafu uongozi wa NAUTS na USUD, lakini ni sahihi pia kusema kwamba malumbano yaliyosababisha zahama hii yalianza wakati yeye ndiye kiongozi. Hivyo hatuna budi kumuona kama kiongozi mkuu wa harakati hizo za wakati huo.
Ni vyema kukumbushana pia kwamba wakati NAUTS inaasisiwa na Joseph Sinde Warioba mwaka 1965, nasi tukajiunga kutoka mikoa yote ya Tanzania, ulikuwa ni umoja rafiki sana na serikali na ambao haukuwa na ugomvi na sera za serikali, lakini chini ya Sitta na wale waliomfuatia, mambo yalikuwa yamebadilika na kuzaa hali ya uhasama.
Sitta alirejea chuoni mwaka 1969 kumalizia mwaka wake wa tatu, wakati mimi nikiingia mwaka wa kwanza, na katika mwaka huo hakujihusisha sana na siasa. Mwaka uliofuatia alihitimu na kwenda kufanya kazi kama mwanasheria wa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC), na baada ya miaka michache akawa mbunge wa Urambo na waziri chini ya Mwalimu Nyerere yule yule. Tangu wakati huo hadi anaanza kuugua amekuwa katikati ya harakati zote za kisiasa, akibadilishwa kutoka wizara hadi wizara, ukuu wa mkoa, ukuu wa Mamlaka ya Kustawisha Makao Makuu (CDA), Kituo Cha Uwekezaji cha Taifa (TIC), u-Spika na kadhalika.
Mwaka 1995, Sitta alikuwa msitari wa mbele kabisa katika kuwasukuma wale waliojulikana kama Boyz-ll-Men kutafuta uteuzi wa CCM kugombea urais. Hawa ni Jakaya Mrisho Kikwete na Edward Ngoyai Lowassa, ambao walitengenezewa mkakati wa pamoja wa kutafuta nafasi hiyo ndani ya CCM, Sitta akiwa ni miongoni mwa wasuka mikakati wakuu.
Mwaka huo aliyeshinda alikuwa Benjamin William Mkapa, lakini wawili hawa walikuwa na nafasi ya kujaribu tena mwaka 2005, safari hii ikijulikana kwamba nafasi ya urais ni nafasi ya Kikwete na Lowassa akiwa ni meneja mkuu wa kampeni, akitaraji kuja kugombea mwaka 2015, kama sio 2010.
Kati ya Kikwete, Lowassa na Sitta ulitokea mvurugano na kutoelewana katika mikakati ya masafa marefu. Nani awe waziri mkuu, ambaye atapewa nafasi kubwa ya kupokea kijiti kwa Kikwete, nani awe spika, na uwiano baina ya uwaziri mkuu na u-spika ukoje? Nani anakuwa na nafasi kubwa zaidi kuliko mwingine inapokuja kutafuta mrithi wa Kikwete?
Ndani ya kambi ya Lowassa wamo watu walioamini kwamba minyukano hii ndiyo ilimfanya Spika Samuel Sitta akaamua kushabikia kile kilichoitwa Kashfa ya Richmond, ambayo hatimaye ilimng’oa Lowassa katika kile kilichoonekana kama njama iliyosukwa kwa ushirikiano baina ya Kikwete na Sitta.
Ule ubia uliokuwa umejengeka na kuwaweka pamoja Sitta, Lowassa na Kikwete mwaka 1995 ulikuja kuvunjika vipande vipande mnamo mwaka 2007, mhanga mkuu akiwa ni Lowassa. Kamba iliyotumika ni “kashfa” ya Richmond, na “nyonganyonga” akiwa ni Spika Sitta.
Lakini Sitta mwenyewe naye hakuweza kwenda mbali sana kwani ilipofika zamu nyingine ya kuwania u-spika, njama zilisukwa ndani ya chama chake kwamba zamu hii spika awe mwanamke, na kwa sababu haikuwa rahisi kwa Sitta kubadilisha jinsia, akawa ametoswa na nafasi yake ikachukuliwa na Anne Makinda.
Mwishoni kabisa, shughuli kuu aliyohusika nayo Sitta ilikuwa kuandika rasimu ya katiba iliyoshonwashonwa kwa kuunganisha vipande vya vitambaa visivyofanana, kwa lengo moja tu, kuikataa rasimu inayoitwa ya Joseph Warioba, rasimu iliyotokana na mchakato mrefu na mpana uliowahusisha wananchi wengi.
Tume ya Warioba ilifanya kazi nzuri, kazi ngumu lakini nzuri, lakini ilipopeleka mapendekezo yake kwa tajiri wake, Rais Jakaya Kikwete, rais akawa hana ubavu wa kusimamia mapendekezo ya tume yake mwenyewe. Akaenda mbele ya “Bunge la Katiba” chini ya mwenyekiti Sitta, na akaiponda vilivyo “Rasimu ya Warioba,” na kuiacha mchangani.
Ukigeugeu wa Kikwete ulisaidia kumpa Sitta nafasi nyingine ya kuicheza siasa kwa mtindo aliokuwa anaujua vyema. Lakini papo hapo, ilizaa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ulioanza kuratibu shughuli za vyama vya upinzani kutetea upatikanaji wa katiba ya kweli ya wananchi. Kwa sasa nchi imekwama, na haionekani kama utawala wa sasa unayo hamu ya kuingia tena katika malumbano ya kikatiba. Mwelekeo wa sasa ni utawala wa kiimla. Hasara iliyoingizwa nchi hii ni kubwa mno, na pasi na shaka siku moja wale wenye akili watatambua hivyo.
Katika siasa kama zetu, ambazo hazina msingi wa kifalsafa au kiiitikadi, Sitta alikuwa mchezaji nyota mithili ya Maradona. Aliweza kutunga na kusuka mikakati ya kuwahusisha watu wa silka tofauti na masilahi yaliyosigana alimradi lengo la muda uliopo lifanikiwe.
Uzuri wa utamaduni kama huu, kama una uzuri wowote, ni kwamba kila mmoja anacheza mchezo huo huo, na mwisho wa siku kunakuwa hakuna wa kumnunia mwenziwe. Unamnunia mwenzio kwani wewe ulikuwa unacheza mchezo gani ulio bora kuliko hiyo ya wenzako? Waswahili wanasema ni mchezo wa nzi: Wewe unajua miguu ya mbele, wenzako miguu ya nyuma. Na hivyo gurudumu la siasa za Waafrika linavyokwenda, mbele ama nyuma, lakini mara nyingi nyuma.
Sitta ametutoka, lakini historia yake tutabaki nayo. Kama tunapenda kujifunza kuhusu siasa za nchi hii na jinsi zinavyochezwa, hatuna budi kujifunza kutokana na maisha yake. Alikuwa ni mnyama wa kisiasa aliyeishi siasa, akapumua siasa, akala siasa, akanywa siasa. Kama mchango wake ulikuwa na msaada kwa nchi au la, tutajuzwa kadiri tutakavyomsoma na kumtafakari. Tunachoweza kufanya ni kumwombea Samuel John Sitta mapumziko mema ya milele. Amina.
Chanzo: Gazeti la Raia Mwema
Bonyeza Play Hapa Chini Kuona Walichofanya Bilnass na Rosa Ree:
Saluti kwa Jenelali Ulimwwngu, Sakuti tena!
ReplyDelete